Maelezo kuhusu Coronavirus kutoka COVID-19 Health Literacy Project na Harvard Health Publishing

Imetengenezwa na COVID-19 Health Literacy Project kwa kushirikiana na Harvard Health Publishing. Tarehe ya uhakiki: 23/3/20.

[English version also available for download – scroll to bottom for links]


Maana ya ugonjwa wa Corona, kwa jina la kitaalamu “COVID-19”

  • COVID-19 ni ugonjwa wa kuambukiza ambao unaleta madhara katika mfumo wa upumuaji.
  • Maambukizi haya yaligundulika kwa mara ya kwanza huko Wuhan, China.
  • Idadi kubwa ya watu wenye maambukizi huonyesha dalili chache au kutokuwa na dalili kabisa.
  • Ugumu wa kupumua, homa ya mapafu (Nimonia), viungo vya ndani ya mwili kushindwa kufanya kazi, na pia vifo huweza kutokea.

Njia za maambukizi ya Ugonjwa huu wa COVID-19

  • Kutoka kwa mtu mmoja kwenda kwa mwingine: Unaweza kupata maambukizi kutoka kwenye matone ya chafya au kikohozi cha mgonjwa aliyeko umbali wa futi sita au karibu.
  • Kupitia vifaa mbali mbali: Unaweza kupata maambukizi kwa kushika vifaa/vitu vilivyoshikwa na mtu mwenye maambukizi na baadaye kugusa/kushika sehemu za uso kama mdomo, pua na macho. Mfano mzuri ni vitasa vya mlango, meza, simu, and sehemu zinashikwa na watu wengi kama siti za kwenye daladala na bodaboda.

Je, ninaweza kupata COVID-19?

Ndiyo. Unaweza kupata maambukizi ya Corona kama:

  • Unaishi na mtu mwenye maambukizi
  • Unamhudumia mtu mwenye maambukizi
  • Ulikutana na kugusana na mtu mwenye maambukizi
  • Ulishika kifaa/kitu kilichoshikwa na mtu mwenye maambukizi

Unaweza kuwa kwenye hatari ya maambukizi zaidi kama umesafiri maeneo mbali mbali duniani katika miezi ya hivi karibuni, wewe ni mtoa huduma ya afya, au ulikuwa katika nchi zenye maambukizi mengi ya Corona (COVID-19).

Dalili za ugonjwa wa COVID-19

  • Dalili zinazoonekana kwa wingi: Homa, kikohozi kikavu, kupungukiwa/kuishiwa pumzi
  • Dalili zisizoonekana kwa wingi: Uchovu, maumivu ya misuli na viungo vya mwili, koo kuwasha, maumivu ya kichwa

Tofauti kati ya COVID-19 na mafua

  • Dalili za ugonjwa wa corona (COVID-19) na mafua hufanana lakini virusi vinavyosababisha magonjwa haya ni tofauti.
  • Virusi vinavyosababisha ugonjwa wa conona husambaa kwa urahisi na husababisha madhara makubwa kwenye mwili na vifo. Pia, ugonjwa wa corona hauna dawa au chanjo ya kujikinga ukilinganisha na ugonjwa wa mafua.

Jinsi ya kujikinga na kuwakinga wengine

  • Zingatia kutokushika sehemu za usoni, kwa mfano macho, pua na mdomo
  • Tumia leso au tishu pale unapokohoa au kupiga chafya na hakikisha unatupa tishu kwenye debe la taka na kufua leso ili kupunguza maambukizi.
  • Zingatia usafi wa sehemu zinazoguswa kwa wingi, mfano vitasa vya mlango.
  • Zingatia kuosha mikono mara kwa mara kwa maji yanayokiririka na sabuni kwa muda usiopungua sekunde 20. Pia unaweza kutumia dawa ya kuosha mikono (sanitizer) yenye kemikali ya alcohol ya asilimia 60% pale ambapo hauna maji na sabuni kwa ukaribu.
  • Kaa nyumbani na epukana na sehemu zenye misongamano ya watu isiyokuwa ya lazima.

Nifanyeje ninapojisikia kuumwa?

  1. Ni vyema kukaa nyumbani na kuwasiliana na daktari kwa simu. Kama utapata ugumu wa kupumua, kizunguzungu au kuhisi kuchanganyikiwa, au pale ambapo utaona mdomo au uso unabadilika rangi na kuwa bluu, piga simu nambari 0800 110 124 au 0800 110 125 ili upate huduma mara moja.
  2. Watu wengi wenye maambukizi na dalili zisizo kali huweza kujiuguza na kuponea wakiwa nyumbani. Pale endapo itakulazimu kwenya hospitali, ni vyema kuwapigia simu kwanza kabla ya kwenda na kutotumia usafiri kama dalala.

Nini cha kufanya iwapo una maambukizi au unahisi umepata maambukizi

Je, nitarajie nini? Je, nimuone daktari wakati gani?

  • Wengi wanaoshikwa na ugonjwa wa COVID-19 hupona. Dalili kwa watu wenye umri wa chini ya miaka 60 na wenye afya nzuri ni kama zile za
    mafua: Homa (zaidi ya 38°C), kikohozi kikavu, kuwashwa koo, na uchovu wa mwili kwa wiki mbili.
  • Pale unapoona dalili za awali, wasiliana na daktari au mtoa huduma ya afya au piga simu nambari 0800 110 124 au 0800 110 125. Ni muhimu kuwaeleza endapo ulikutana na mtu mwenye maambukizi ya COVID-19.
  • Wataalamu watakupa maelekezo ya wapi pa kwenda ili kupata vipimo.
  • Kutokana na ufinyu wa vipimo kwa sasa, daktari wako anaweza kushauri ubaki nyumbani kwa siku 14 au zaidi iwapo umepata maambukizi.
  • Watu wenye umri wa miaka 60 na zaidi na wale wenye magonjwa mbali mbali, mfano: matatizo ya moyo, ugonjwa wa mapafu au kansa huweza kuona dalili zenye athari kubwa zaidi. Vile vile, vijana na watu wenye afya nzuri huweza kuona dalili zenye athari kubwa pia.
  • Dalili hizi zinaweza kupelekea mgongwa akalazwa hospitalini. Wasiliana na daktari au mtoa huduma ya afya au piga simu nambari 0800 110 124 au 0800 110 125 au KABLA ya kwenda hospitalini.

Wasiliana na daktari au mtoa huduma ya afya haraka sana ukiona dalili zifuatazo:

  • Ugumu wa kupumua
  • Kusikia kizunguzungu au hali ya usingizi au kuchanganyikiwa
  • Mdomo na uso kubadilika rangi na kuwa bluu

Ugonjwa huu unatibiwaje?

PowerPoint Presentation

  • Kwa sasa, hakuna tiba maalumu ya ugonjwa wa COVID-19. Wagonjwa wengi huanza kupata nafuu baada ya kupumzika na kunywa maji kwa wingi. Dawa ya Panadol huweza kusaidia kupunguza homa kali na kutuliza maumivu ya misuli.
  • Iwapo utakuwa na dalili kali/zenye athari kubwa na ukafikishwa hospitalini, madaktari wataandaa mpango maalumu wa kukutibu kulingana na afya yako.

Nitawakingaje wengine na ugonjwa huu?

Pale ambapo utahisi umepata maambukizi ya COVID-19, ni muhimu kukaa nyumbani.

Kwa kawaida, itakuchukua wiki mbili za kujitenga na kukaa nyumbani. Baada ya kipindi hiki, maamuzi ya kuendelea na shughuli za kawaida ni vyema yakachukuliwa kwa ushauri wa daktari.

Zingatia kuto kukaa karibu na watu.

Tumia chumba maalumu na vifaa tofauti na watu wengine ili kudhibiti maambukizi kuenea. Tumia barakoa (mask) kama unayo ili kuwakinga wengine na maambukizi.

Zingatia usafi wa mikono.

Funika mdomo na pua kwa leso au tishu au kiwiko unapo kohoa au kupiga chafya. Jizuie kugusa sehemu za uso kama macho, pua na mdomo. Osha mikono mara kwa mara kwa kutumia sabuni na maji yanayo tiririka kwa angalau sekunde 20. Tumia dawa ya kuosha mikono (sanitizer) yenye alcohol isiyopungua asilimia 60%.

Zingatia usafi wa nyumba.

Usishirikiane vitu vya binafsi. Safisha sehemu zinazotumiwa na kuguswa kwa wingi (meza, vitasa vya milango, vyoo, simu, kompyuta, swichi za taa n.k) kila siku. Tumia dawa maalumu za kusafisha zenye alcohol isiyopungua 70%, bleach iliyo changanywa na maji, au sabuni maalumu za kufanyia usafi.


Zuia kuenea kwa maambukizi ya COVID-19

Kaa nyumbani, isipokuwa kupata matibabu!

Hakikisha unakaa umbali wa futi 6 kutoka kwa watu wengine hata kama hawaonekani kuwa wagonjwa. Hakikisha una fuata maelekezo ya serikali yako kuhusiana na kukaa nyumbani.

Osha mikono kwa maji na sabuni kwa muda usiopungua sekunde 20 kabla ya kula au kuandaa/kupika chakula, na baada ya kupiga chafya, kusafisha pua, au pale unapotoka sehemu ya hadharani kama sokoni au kazini.

Tumia dawa maalumu ya kuosha mikono (sanitizer) yenye alcohol isiyopungua asilimia 60% endapo hautoweza kuosha mikono kwa maji na sabuni.

Zingatia kutokushika sehemu za usoni mfano macho, pua na mdomo.

Virusi vya COVID-19 vinaweza kutua kwenye sehemu kama meza au kiti na kukaa kwa siku kadhaa. Unaweza kupata maambukizi pale ambapo utagusa sehemu hizi na baadaye kugusa macho, pua au mdomo.

Zingatia usafi wa sehemu zinazoguswa kwa wingi.

Tumia dawa maalumu za kusafisha zenye alcohol isiyopungua 60%, bleach iliyo changanywa na maji, au sabuni maalumu za kufanyia usafi, kusafisha/kupangusa vitasa vya mlango, meza, simu, funguo, tablets, kompyuta, rimoti za Runinga n.k.

Funika mdomo ukikohoa na kupiga chafya kwa kutumia leso, tishu na kiwiko chako.

Virusi vya COVID-19 husambaa/huenea kupitia matone ya chafya au kikohozi cha mtu mwenye maambukizi.

Weka mpango wa namna ya kujilinda wewe na uwapendao.

Watu wazima na wale wenye matatizo ya kiafya wako katika hali hatarishi zaidi. Ni vyema wakawasiliana na watoa huduma wa afya kuhusu namna ya kujilinda. Andaa orodha ya mawasaliano ya watu wa karibu wa kutafutwa wakati wa dharura. Tenga sehemu maalumu katika nyumba kwa wanafamilia watakaopata maambukizi.

FANYA

  • Kaa nyumbani isipokuwa kupata matibabu. Kama una dalili kali, piga simu 0800 110 124 au 0800 110 125.
  • Osha mikono yako na sabuni na maji kwa angalau sekunde 20 (au tumia sanitizer yenye alcohol angalau 60%).
  • Funika mdomo ukikohoa na kupiga chafya na kiwiko chako.
  • Kwa habari kuhusu COVID-19 tembelea tovuti ya COVID-19 ya idara ya afya ya eneo lako, CDC, na WHO.
  • Ongea na Ndugu, Jamaa na Marafiki kupita simu yako ya mkononi.

USIFANYE

  • Usiondoke nyumbani kwako au kuwa katika vikundi kwa sababu zisizo muhimu.
  • Usivae barakoa (mask) au glovu isipokuwa wewe ni mgonjwa au unamjali mtu mgonjwa.
  • Usikohoe mikononi mwako.
  • Usikusanye habari kutoka tovuti au vyombo vya habari visivyothibitishwa.
  • Usitembelee ndugu, jamaa, marafiki na familia kwa sababu unaweza kuweka kila mmoja katika hatari kubwa ya kuambukizwa.

Imetengenezwa na COVID-19 Health Literacy Project kwa kushirikiana na Harvard Health Publishing. Tarehe ya uhakiki: 23/3/20.


Download Swahili posters:


Download English posters:

Created by the COVID-19 Health Literacy Project in collaboration with Harvard Health Publishing. Date of last review: 23/3/20.

Previous ArticleNext Article
Al-Amin founded Vijana FM in 2009. With over a decade of experience in communications, design and operations, he now runs a digital media consulting agency - Lateral Labs - in Dar-es-Salaam.

This post has 2 Comments

2

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Send this to a friend